Alhamisi, 24 Novemba 2016

TEMESA YATAKIWA KUHARIKISHA MIFUMO YA KIELETRONIKI

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), Dkt. Mussa Mgwatu akieleza utendaji kazi kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, alipotembelea Wakala huo, jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akitoa maelekezo kwa Uongozi wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), alipokagua karakana ya Wakala huo, jijini Dar es Salaam

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akiteta na mmoja wa madereva wa Serikali katika karakana ya TEMESA, alipokagua karakana ya Wakala huo, jijini Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), Dkt. Mussa Mgwatu akisisitiza jambo wakati  Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, alipotembelea Wakala huo, jijini Dar es Salaam

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akisisitiza jambo wakati akiongea na wafanyakazi wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), Kanda ya Dar es Salaam na Pwani (hawapo pichani) alipokutana nao jijini Dar es Salaam.

Wafanyakazi wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), Kanda ya Dar es Salaam na Pwani, wakimsikiliza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (hayupo pichani) alipokutana nao jijini Dar es Salaam kuwaeleza mikakati ya Serikali kwa Wakala huo.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa ameutaka uongozi wa Wakala wa Ufundi na Umeme nchini (TEMESA), kuharakisha zoezi la uwekaji wa mifumo madhubuti ya kieletroniki katika vituo vyake ili kuongeza ufanisi katika utendaji kazi.

Hayo ameyasema wakati alipokuwa akizungumza na wafanyakazi wa Wakala huo wa kanda ya Dar es Salaam na Kibaha ambapo amesema mifumo hiyo ikikamilika itadhibiti na kuongeza mapato kwa uharaka.

"Kamilisheni haraka hiyo mifumo ili kuweza kuboresha utendaji kazi wenu na wateja waweze kufurahia huduma ya uhakika na haraka", amesema Prof. Mbarawa.

Aidha ameongeza kuwa Wakala unatakiwa kupunguza idadi ya wafanyakazi wasio na tija na kuajiri wafanyakazi wachache wenye sifa kulingana na mahitaji halisi yanayohitajika katika vituo vyao.

“Msilete watumishi kwa sababu mnawajua, chukueni watu mnaowahitaji kulingana na kazi zenu ili muweze kuifanya TEMESA iwe na hadhi inayostahili”, amesisitiza Prof. Mbarawa.

Kwa upande wa ongezeko la gharama za vipuri vya magari zisizoendana na bei ya soko na kupelekea kupunguza wateja kwa Wakala huo, Prof. Mbarawa ameuagiza uongozi kuwaondoa wasambazaji wote wanaoongeza gharama hizo ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.

Naye Mtendaji Mkuu wa TEMESA, Dkt Mussa Mgwatu amesema Wakala huo utaanza kutumia mfumo wa kitehama kwa ajili ya kutunza taarifa za matengenezo ya magari na utafanywa kwa awamu ukianzia karakana ya Dar es Salaam na Kibaha.

Dkt. Mgwatu ameongeza kuwa Mfumo huo utaweza kufatilia mwenendo wa gari na kutuma ujumbe mfupi kwa njia ya simu (sms) kwa wateja kuwakumbusha siku za matengenezo ya magari, wateja kujua mwenendo wa matengenezo na Wakala kutambua madeni yaliyoko kwa wateja.

Katika kuboresha utendaji kazi na kuongeza ufanisi amemuhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuunda muundo mpya ambao utabainisha majukumu ya kila kada kwa uwazi ili kusaidia kutoingiliana kazi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni