Jumanne, 27 Septemba 2016

BARABARA ZA ARUSHA KUKAMILIKA MWAKANI



Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akielekea kukagua kingo za Daraja la Themi linalojengwa katika barabara ya Sakina-Tengeru yenye urefu wa KM 14.1 jijini Arusha.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akipata maelezo kutoka kwa Mhandisi Mkazi Shin Pil Soo wakati akikagua Daraja la Nduruma lenye urefu wa mita 60 linalojengwa katika barabara ya Sakina-Tengeru yenye urefu wa KM 14.1 jijini Arusha.


Muonekano wa juu wa Daraja la Nduruma lenye urefu wa mita 60 linalojengwa katika barabara ya Sakina-Tengeru yenye urefu wa KM 14.1 jijini Arusha.


Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoa wa Arusha Eng. Johnny Kalupale (katikati), akifafanua jambo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kulia), alipokagua ujenzi wa barabara ya Sakina-Tengeru yenye urefu wa KM 14.1 na barabara ya Arusha mchepuo (bypass), yenye urefu wa KM 42.4 jijini Arusha.


Muonekano wa barabara ya Sakina-Tengeru yenye urefu wa KM 14.1 ambayo upanuzi wake unaendelea jijini Arusha.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akishiriki kikamilifu katika uwekaji wa kifusi cha tabaka la juu la zege kabla ya kumwaga lami katika barabara ya Sakina-Tengeru yenye urefu wa KM 14.1 ambayo ujenzi wake unaendelea.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akisalimiana na baadhi ya wananchi wakati alipokagua ujenzi wa barabara ya Sakina-Tengeru yenye urefu wa KM 14.1 ambayo ujenzi wake unaendelea.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akitoa maelekezo kwa Meneja wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini (TAA), mkoa wa Arusha Bw. Elipid Tesha namna bora ya kupunguza msongamano uwanjani hapo.



Sehemu ya eneo la kuegeshea ndege katika Uwanja wa Ndege wa Arusha ambao unakabiliwa na ufinyu wa maegesho ya ndege ambapo Serikali iko katika hatua za kuuboresha.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amemtaka mkandarasi M/S Hanil Jiangsu J/V anayejenga barabara ya Sakina-Tengeru yenye urefu wa KM 14.1 na barabara ya mchepuo (Arusha bypass) yenye urefu wa KM 42.4 kuhakikisha barabara hizo zinakamilika ifikapo mwezi Machi na Oktoba mwakani.
 
Profesa Mbarawa amesema hayo mara baada ya kukagua ujenzi barabara hizo na kujiridhisha na hatua iliyofikiwa kwa barabara zote.

“Meneja hakikisha ujenzi wa barabara hizi unakwenda sambamba na ujenzi wa sehemu ya barabara inayoelekea Ikulu ya mjini Arusha ili kuiunganisha vizuri barabara hiyo kwa kiwango cha lami”, amesema Prof. Mbarawa.

Amemtaka Mkuu wa Wilaya ya Arusha Bw. Gabriel Daqarro kushirikiana na Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoani humo kuhakikisha maji yanayopita kwenye madaraja yaliyopanuliwa kufuatia ujenzi unaoendela hayasababishi mafuriko kwenye makazi ya wananchi.

Kwa upande wake Meneja wa TANROADS mkoa wa Arusha Eng. Johnny Kalupale amemhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuwa ujenzi wa barabara mkoani Arusha utakamilika kwa wakati na ubora unaotakiwa.

“Tumejipanga kuhakikisha barabara ya Sakina-Tengeru na ile ya mchepuo zote zitakamilika kama ilivyopangwa ili kupunguza msongamano hali itakayovutia ongezeko la watalii na hivyo kukuza uchumi wa mkoa wa Arusha”, amesema Eng. Kalupale.

Katika hatua nyingine Waziri Prof. Mbarawa amekagua uwanja wa ndege wa Arusha na kusisitiza kuwa nia ya Serikali ni kuupanua uwanja huo ambao ni wa nne kwa uingizaji wa mapato nchini ili kuondoa msongamano uliopo sasa.

“Wakati Serikali tunajipanga kuongeza uwanja huu na nyinyi mjipange kuongeza mapato ili jitihada za Serikali ziendane na ubunifu wa watendaji”, amesisitiza Prof. Mbarawa.

Naye Meneja wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini (TAA), mkoa wa Arusha Bw. Elipid Tesha amesema uwanja huo ambao ni kitovu cha utalii katika ukanda wa Kaskazini ukiongezwa utaruhusu ndege nyingi kutua na hivyo kuuongezea mapato ambapo kwa sasa takribani miinuko 110 ya ndege hufanyika kila siku katika uwanja huo.

“Kwa sasa uwanja wa ndege wa Arusha una barabara ya kurukia yenye urefu wa KM 1.6 hali inayosababisha baadhi ya ndege kushindwa kuutumia ila mkakati wa uwanja huo ni kuuongeza uwe na urefu wa KM 2.5”, amesisitiza Bw. Tesha.

Uwanja wa Ndege wa Arusha uliojengwa mwaka 1956 ikiwa ni mkakati wa kuboresha huduma za utalii katika mkoa huo uko KM 7 kutoka Arusha Mjini na una eneo la ekari 280 na uzio unaoimarisha usalama wakati wote.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni