Jumatano, 7 Septemba 2016

KIVUKO CHA MV MAGOGONI CHAANZA KAZI RASMI




Mkuu  wa Jeshi la Majini (Navy, Meja Jenerali Rogastian Laswai (kulia) akitoa maelezo Kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga (Wa kwanza kushoto) kuhusu huduma za usafiri wa majini katika Kivuko cha Mv. Magogoni.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga (Wa nne kushoto) akiwa pamoja na watendaji wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) wakivuka kuelekea upande wa Kigamboni kwa kutumia usafiri wa Mv. Magogoni.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga akishuka kutoka katika kivuko cha Mv. Magogoni.

Wakazi wa Kigamboni wakielekea kupanda  kivuko cha Mv. Magogoni mara baada ya kuanza kutoa huduma za usafiri kati ya Magogoni  na Kigamboni.

Muonekano wa Kivuko cha Mv. Magogoni kikiwa majini mara baada ya ukarabati wake kukamilika.
Kivuko cha MV. Magogoni kimepokelewa na kuanza kazi rasmi ya kutoa huduma za usafirishaji kati ya eneo la Kigamboni na Magogoni mara baada ya kukamilika kwa ukarabati wake mkubwa.
 
Akizungumza jijini Dar es salaam mara baada ya kukipokea kivuko hicho Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga amesema kuwa kukamilika kwa ukarabati wa kivuko hicho kutaimarisha huduma za usafirishaji kwa wakazi wa Kigamboni.

“Kivuko kimeanza kazi rasmi, matumaini yangu adha ya usafiri kwa wananchi wa Kigamboni na Magogoni itapungua”, amesema Eng. Nyamhanga.

Aidha, Katibu Mkuu huyo amebainisha ujenzi wa kivuko kingine cha tatu  kwa ajili ya kuboresha huduma ya usafiri ili kuweza kusaidiana na vivuko vingine vinavyofanya kazi katika maeneo hayo.

Amefafanua kuwa kivuko hicho kinatarajiwa kukamilika mwezi Novemba mwaka huu na kitakuwa na uwezo wa kubeba abiria 800 na magari 22 kwa wakati mmoja.

Kuhusu utoaji huduma katika vituo vya kukatia tiketi katika maeneo hayo Eng. Nyamhanga amemuagiza Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Eng. Manase Ole Kujan kuboresha mfumo wa kukatia tiketi kuwa wa njia ya kadi ambayo itamruhusu mtumiaji kukata tiketi kwa kipindi anachotaka.

“Hakikisheni kuwa mfumo uliopo sasa unabadilika na kuwa wa kadi ili kumrahisishia mtumiaji wa huduma zenu na kurahisisha katika ukusanyaji wa mapato”, amesisistiza Eng. Nyamhanga.

Naye, Kaimu Mtendaji Mkuu wa TEMESA, Eng. Manase Ole Kujan amesema kuwa ukarabati wa kivuko hicho umegharimu kiasi cha shilingi Bilioni 1.1 ambapo ukarabati mkubwa umefanyika kwenye injini na mfumo wa umeme.

Eng. Kujan amefafanua kuwa Serikali ina mpango wa kufanya upanuzi  wa eneo la kupumzikia abiria sehemu ya Kigamboni  ambapo jumla ya nyumba 7 zitaathirika katika mchakato huo.

“Nyumba hizi zinaendelea kufanyiwa tathmini na taratibu za kuwalipa fidia zinaendelea”, amesema Eng. Kujan.

Katika kuhakikisha huduma za vivuko zinaimarika nchini, Serikali kupitia TEMESA inatarajia kukifungua kivuko cha Mv Pangani II mkoani Tanga mwezi huu na kununua kivuko kingine kipya ambacho kitatoa huduma kati ya Kigongo na Busisi mkoani Mwanza.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni