Alhamisi, 6 Oktoba 2016

TEMESA YATAKIWA KUONGEZA MAPATO


Muonekano wa kivuko kipya cha MV Kazi kikiwa katika hatua za awali za ujenzi wake. Kivuko hicho kinatarajiwa kukamilika mwezi Disemba mwaka huu.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, akitoa maelekezo kwa Watendaji wa Kampuni ya Songoro wanaojenga kivuko kipya cha MV. Kazi, kinachojengwa katika yadi ya Bandari jijini Dar es Salaam, mara baada ya kutembelea na kujionea ujenzi wake. Kivuko hicho kipya kinatarajiwa kukamilika mwezi Disemba mwaka huu.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, akiongea na mafundi wa wa Kampuni ya Songoro wanaojenga kivuko kipya cha MV. Kazi, kinachojengwa katika yadi ya Bandari jijini Dar es Salaam, mara baada ya kutembelea na kujionea ujenzi wake. Kivuko hicho kipya kinatarajiwa kukamilika mwezi Disemba mwaka huu.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, akitoa maelekezo kwa Watendaji wa Wakala wa Ufundi na Umeme nchini (TEMESA), alipotembelea eneo la Kivukoni. Katikati ni Mkuu wa Kivuko upande wa Dar es Salaam, Eng. Lukombe King’ombe.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, akiongea na mwanafunzi Arafat Kondo wakati alipotembelea kivuko cha MV. Kigamboni kujionea utendaji wake.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, akishuka kwenye pantoni mara baada ya kukagua utendaji wa kivuko cha MV. Kigamboni.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, akisikiliza taarifa ya matumizi ya mafuta kutoka kwa Mhandisi wa Wakala wa Ufundi na Umeme  nchini (TEMESA) alipotembelea kivuko cha MV. Kigamboni.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa ameuagiza uongozi wa Wakala wa Ufundi na Umeme nchini (TEMESA), kuhakikisha wanaweka mipango madhubuti ya kuongeza mapato katika vivuko vya MV. Kigamboni na MV. Magogoni kutoka Shilingi Milioni 14 ambazo zinakusanywa hivi sasa hadi kufikia Milioni 19 kwa siku.

Akizungumza jijini Dar es Salaam mara baada ya kukagua vivuko hivyo na kuongea na Mtendaji Mkuu wa TEMESA Dkt. Mussa Mgwatu Prof. Mbarawa amesema kuwa kipimo cha utendaji huo utafanyika ndani ya miezi minne ili kuongeza ufanisi katika utendaji kazi wa vivuko hivyo na kuweza kufikia malengo.

“Hatushindwi kutafuta mtu mwingine mwenye ujuzi na utendaji wa kazi uliotukuka, kama lengo la kukusanya milioni 19 halitafikiwa basi mkuu wa kivuko atafute kazi nyingine, na tutafanya hivyo mpaka tuhakikishe tunapata atayeweza kukusanya kiwango hiki”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.

Prof. Mbarawa ameutaka Wakala huo kuboresha mifumo ya ukusanyaji wa mapato katika vivuko hivyo na kuwa wa kieletroniki ili kudhibiti ubadhilifu unaofanywa na watumishi wasio waaminifu wakati wa utoaji huduma.

Katika hatua nyingine Prof. Mbarawa amejionea maendeleo ya ujenzi wa kivuko kipya cha MV. Kazi  nakusema kuwa kivuko hicho kitarahisisha usafiri kwa wakazi wa Kigamboni.

Aidha, amemtaka mkandarasi wa Kampuni ya Songoro Marine Transport kumaliza utengenezaji wa kivuko hicho ifikapo Mwezi Disemba mwaka huu ili watanzania wapate huduma bora za usafiri.

Ameongeza kuwa Kampuni hiyo ihakikishe kuwa inasimamia upatikanaji wa injini za Kivuko hicho kwa wakati ili kusaidia ujenzi huo kukamilika kwa muda uliopangwa.

“Nina imani na kasi mnayokwenda nayo, na nina uhakika Kivuko hiki kitamalizika kwa wakati naomba muwe waangalifu na kuhakikisha kwamba injini za kivuko hiki zinawasili mapema”, amesisitiza Prof. Mbarawa.

Naye Mkurugenzi wa Karakana ya Dar es Salaam wa Kampuni ya Songoro Marine, Saleh Songoro amesema kuwa ujenzi wa Kivuko cha MV Kazi upo katika hatua nzuri ambapo kwa sasa wanakamilisha kazi ya kuchomea milango katika kivuko hicho.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TEMESA Dkt. Mgwatu amemuhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuwa maagizo yote yatatekelezwa ikiwemo kutatua changamoto mbalimbali zinazokabili Wakala huo.

Dkt. Mgwatu amewataka wananchi kuwa na subira wakati kivuko cha MV. Kazi kinamalizika kujengwa kwani kitapunguza kama sio kuondoa msongamano uliopo sasa katika maeneo ya Magogoni na Kigamboni. 

Ujenzi wa kivuko cha MV Kazi ulianza Mwezi Juni mwaka huu ambapo kina uwezo wa kubeba tani 170 sawa na watu 800 na magari 22 kwa wakati mmoja.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni