Jumatano, 7 Juni 2017

WAZIRI MBARAWA APOKEA KIVUKO CHA MV KAZI

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa (kushoto) akitoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Songoro Marine Transport Ltd. Bw. Major Songoro (kulia)  wakati wa makabidhiano ya Kivuko cha MV. KAZI mapema hii leo jijini Dar es Salaam, katikati ni Mtendaji Mkuu toka Wakala wa Ufundi na Umeme  (TEMESA) Dkt. Mussa  Mgwatu.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa (kulia) akizungumza na baadhi ya wananchi waliopanda Kivuko cha MV. KAZI mara baada ya kukabidhiwa kwa Serikali toka kwa  Kampuni ya Songoro Marine Transport Ltd. Iliyokuwa ikikijenga Kivuko hicho.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliana Prof. Makame Mbarawa (kushoto) akizungumza na mmoja  ya mkazi wa Kigamboni wakati wa kukabidhiwa kivuko cha MV. KAZI kwa Serikali toka kwa Kampuni ya Songoro Marine Transport Ltd. Iliyokuwa ikikijenga Kivuko hicho.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa (kushoto) akifurahia jambo na  mmoja  ya mkazi wa Kigamboni wakati wa kukabidhiwa Kivuko cha MV. KAZI kwa Serikali toka kwa Kampuni ya Songoro Marine Transport Ltd. Iliyokuwa ikikijenga kivuko hicho.

Baadhi ya wananchi wakiteremka katika Kivuko cha MV. KAZI mara baada ya kukabidhiwa rasmi kwa Serikali mapema hii leo Magogoni jijini Dar es Salaam toka Kampuni ya Songoro Marine Transport Ltd. Iliyokuwa ikikijenga Kivuko hicho.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa amepokea Kivuko cha MV Kazi kutoka kwa Kampuni ya kizalendo ya M/S Songoro Marine Transport Boatyard ya Mwanza iliyokuwa inafanya kazi ya ujenzi wa Kivuko hicho mara baada ya ujenzi wake kukamilika.

Akizungumza na wananchi, Prof Mbarawa alisema lengo la Serikali kuongeza Kivuko hicho  ni kuboresha huduma za kusafirisha abiria na magari kati ya Magogoni na Kigamboni.

“Uwepo wa vivuko vitatu kutasaidia utoaji wa huduma kwa wakati na kwa urahisi na ikitokea Kivuko kimoja kimepelekwa kufanyiwa ukarabati huduma zitaendelea kama kawaida bila kuathiri utaratibu wa kawaida”.Alisema Prof Mbarawa.

Ameongeza kuwa ili kuendana na kasi ya Mhe. Rais John Magufuli  Wizara yake itaendelea kuboresha huduma za Vivuko katika Mikoa mingine ikiwemo Mkoa wa Lindi , Kivuko cha Pangani, na Kivuko cha Kigongo Busisi Mkoani Mwanza.

Nae Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Dkt. Dkt. Mussa Mgwatu alisema Kivuko cha MV Kazi kimejengwa kulingana na viwango vinavyotakiwa Kimataifa na ukaguzi wake umefanywa na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) na kuthibitishwa kuwa ni salama kwa ubebaji wa abiria na magari.

 Ujenzi wa MV KAZI umegharimu Shilingi Bilioni 7.3 za Kitanzania na kina uwezo wa kubeba abiria 800 magari 22 sawa na jumla ya tani 170. 

Kivuko hicho kimekabidhiwa leo kwa ajili ya kuanza kutoa huduma kati ya Magogoni na Kigamboni Jijini Dar es salaam na kuongeza idadi ya vivuko katika eneo hilo kufikia vitatu.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni