Ijumaa, 31 Machi 2017

PROF. MBARAWA: NEEMA YAJA WAFANYABIASHARA KANDA YA ZIWA

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (katikati), akielekea kukagua Bandari ya Kemondo mkoani Kagera ili kujionea utendaji kazi wake.  Kulia ni Meneja wa Bandari Kanda ya Ziwa, Bw. Abel Moyo.

Meneja wa Bandari Kanda ya Ziwa, Bw. Abel Moyo, akimuonesha Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (Wa pili kushoto), njia ya reli katika bandari ya Kemondo mkoani Kagera, ambayo itaruhusu mizigo itakayokuja kwenye mabehewa kwa njia ya meli iweze kupakuliwa na kupelekwa kuhifadhiwa kwenye maghala.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, akikagua sehemu ya maegesho ya meli katika Bandari ya Kemondo, mkoani Kagera. Bandari hiyo ina upana wa mita 100.

Muonekano wa gati ya meli katika Bandari ya Kemondo, mkoani Kagera.

Kaimu Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), mkoani Kagera Eng. Zephrine Bahyona, akifafanua jambo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa nne kulia), alipokuwa akikagua Kivuko cha Kyanyabasa kinachotoa huduma katika mto Kyanyabasa, mkoani Kagera.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akitoa maelekezo kwa Kaimu Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), mkoani Kagera Eng. Zephrine Bahyona, alipotembelea na kukagua kivuko cha Kyanyabasa kinachotoa huduma katika mto Kyanyabasa, mkoani Kagera.

Muonekeano wa kivuko cha Kyanyabasa kinachotoa huduma katika mto Kyanyabasa, mkoani Kagera. Kivuko hicho kina uwezo wa kubeba watu sitini au magari mawili madogo kwa wakati mmoja.

Imeelezwa kuwa kukamilika kwa ukarabati wa meli ya MV Umoja kutarudisha huduma ya usafirishaji wa mizigo katika kanda ya ziwa kupitia bandari ya Kemondo  iliyopo mkoani Kagera.

Kauli  hiyo imetolewa na  Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, wakati akikagua Bandari hiyo kuangalia maendeleo yake, na kuitaka Mamlaka ya Bandari Nchini (TPA), Shirika la Reli Nchini (TRL), na Kampuni ya Huduma za Meli (MSCL),  kuanza kuandaa Mfumo mmoja wa kutoa Stakabadhi ili kuwarahisishia wateja wake huduma za usafirishaji wa mizigo.

Aidha, Waziri Mbarawa ameitaka TRL kukarabati njia za reli bandarini hapo haraka iwezekanavyo ili kuruhusu mizigo itakayokuja ikiwa kwenye mabehewa kwa njia ya meli iweze kupakuliwa pindi Meli hiyo itaposhusha.

"Serikali imefanya ukarabati wa meli ya MV Umoja ambayo itabeba mizigo ikiwa kwenye mabehewa na reli hii inahitaji ukarabati mapema ipasavyo nawaagiza TRL kufanya ukarabati wa reli ili kusiwepo usumbufu wowote wakati wa kushusha na kupakia mizigo hiyo" , amesema Profesa Mbarawa.

Ameiagiza Mamlaka hiyo kuanza kutafuta tena wateja ambao kwa muda mrefu walikuwa wamepotea kutokana na  bandari hiyo kusuasua kutoa huduma zake kwa muda mrefu.

Kwa upande wake Meneja wa TPA Kanda ya Ziwa Bw. Abel Moyo, amemuahidi Waziri huyo  kutekeleza agizo lake kwa kushirikiana na TRL pamoja na MSCL na kuwahakikishia wafanyabiashara wa kanda ya ziwa  kuwa na matumaini mpya ya kupata usafiri bora na wa uhakika.

Katika hatua nyengine, Waziri Mbarawa ametembelea na kukagua Kivuko cha Kyanyabasa kinachotoa huduma katika mto Kyanyabasa na kumtaka Kaimu Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) mkoani humo, Eng. Zephrine Bahyona,  kutoa huduma bora sambamba na kukusanya mapato ili kuweza kutatua changamoto ndogondogo zinazowakabili.

Naye, Kaimu Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) mkoani humo Eng. Zephrine Bahyona, amezitaja baadhi ya changamoto zinazoathiri utendaji mzuri wa kivuko hicho kuwa ni kukatika kwa magugu maji na hivyo kupelekea kusombwa kwa kivuko.

Waziri Profesa Mbarawa pia amekagua barabara ya Uyovu- Bwanga yenye urefu wa kilometa 45 mkoani Geita na kuridhishwa na kasi ya Mkandarasi wa ujenzi wa barabara hiyo ambapo ujenzi wake kwa sasa umefika asilimia 56.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni