Alhamisi, 25 Agosti 2016

NAIBU WAZIRI ENG. NGONYANI AFUNGUA WARSHA YA WATAALAMU WA ICT

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano  Mhe. Edwin Ngonyani (Mb) akizungumza na wataalamu wa Teknolojia ya habari na mawasiliano (ICT) hawapo pichani wakati akifungua warsha ya   wataalamu wa teknolojia ya habari na Mawasiliano katika ukumbi wa mkutano wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere.  

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano anayesimamia sekta ya Mawasiliano Prof. Faustin Kamuzora akizungumza wakati akimkaribisha Mgeni rasmi Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano  Mhe. Edwin Ngonyani (Mb) ili kufungua warsha ya  wataalumu wa teknolojia ya habari na Mawasiliano.  

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya TEHAMA Mhandisi Samson Mwela akitoa mada   wakati wa warsha  ya wataalamu wa Teknolojia ya habari na Mawasiliano katika ukumbi wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere


Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano  Mhe. Edwin Ngonyani (wa tatu kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa sekta ya mawasiliano   na wataalamu wa teknolojia ya habari na Mawasiliano  Jijini DSM.


TAZARA YAPONGEZWA KWA UKARABATI WA KICHWA CHA TRENI



Meneja wa TAZARA mkoa wa Tanzania Bw. Fuad Abdallah (kulia), akitoa maelezo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa pili kulia), wakati alipokuwa akikagua kichwa cha Treni jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa pili kushoto), akipata maelezo kutoka kwa Mtaalamu (kushoto) namna ya Kichwa cha Treni kinavyofanya kazi wakati alipokuwa akikagua kichwa hicho jijini Dar es Salaam

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (mwenye suti), akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani), mara baada ya kukagua kichwa cha treni ambacho kilikuwa kikifanyiwa ukarabati katika karakana ya TAZARA mkoani Mbeya. Kushoto kwake ni Meneja wa TAZARA mkoa wa Tanzania Bw. Fuad Abdallah.


Serikali imeipongeza Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA), kwa kutekeleza agizo la kukamilisha ukarabati wa kichwa cha Treni ndani ya miezi miwili ambacho kilikuwa kikifanyiwa ukarabati wake  katika karakana ya  Mbeya.

Akiongea mara baada ya kukikagua kichwa hicho katika karakana ya Mamlaka hiyo jijini Dar es salaam, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amesema kukamilika kwake kutasaidia huduma bora na ya uhakika kwa usafirishaji wa mizigo na abiria.

“Nimefurahishwa na uharaka wenu wa utendaji kazi, kwani nilitoa miezi miwili kwa TAZARA kukarabati  kichwa hiki haraka iwezekanavyo kutokana na umuhimu wake”, amesema Waziri Mbarawa.

Aidha, Profesa Mbarawa ametoa wito kwa wafanyakazi wa Mamlaka hiyo kufanya kazi kwa moyo na kwa ufanisi ili kuweza kufufua Mamlaka hiyo ambapo kwa kipindi kirefu ilikuwa na misukosuko mingi.

Naye Meneja wa TAZARA mkoa wa Tanzania Bw. Fuad Abdallah, amemuhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuwa Mamlaka hiyo itaendelea na huduma za usafirishaji wa mizigo na abiria ndani na nje ya nchi.

“Kwa sasa TAZARA inaendelea kuboresha na kuimarisha huduma za usafirishaji wa mizigo kutoka Bandari ya Dar es salaam hadi New Kapiri Mposhi kati ya siku nne hadi saba ukilinganisha na siku zilizopita”, amesema Bw. Fuad.

Kichwa hicho cha Treni kimekarabatiwa kwa gharama ya shilingi Bilioni moja ambapo Serikali imeokoa Bilioni Tisa mpaka Kumi endapo ingenunua kichwa kipya.


Jumanne, 23 Agosti 2016

WAZIRI PROF.MBARAWA AKUTANA NA MKURUGENZI MTENDAJI WA BENKI YA MAENDELEO YA AFRIKA.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa tatu kulia), akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), kanda ya Afrika Mashariki Dkt. Nyamajeje Weggora (wa tatu kushoto), alipomtembelea ofisini kwake Jijini Dar es salaam.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa kwanza kulia) akifafanua jambo kwa wajumbe kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), kanda ya Afrika Mashariki walipomtembelea ofisini kwake Jijini Dar es salaam.

Alhamisi, 18 Agosti 2016

SERIKALI YAJIPANGA KUBORESHA SEKTA YA UCHUKUZI






Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa akipata maelezo kuhusu uboreshwaji wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT),kutoka kwa Mkuu wa Chuo hicho Prof. Zacharia Mganilwa alipokagua chuo hicho jijini Dar es Salaam.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, akikagua moja ya darasa linalotumika kufundishia Marubani wa ndege alipokagua  Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), jijini Dar es Salaam.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa akiongea na wanafunzi wanaosoma kozi ya udereva alipotembelea Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), jijini Dar es Salaam. Kushoto (mwenye tai nyekundu) ni Mkuu wa Chuo hicho Prof. Zacharia Mganilwa.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa akibadilishana uzoefu na makapteni wa meli ya Azam aliposafiri na boti hiyo.


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa akiongea na mmoja wa abiria wanaotumia usafiri wa boti kutoka Dar es Salaam kwenda Zanzibar, na kujionea changamoto mbalimbali zinazowakabili abiria hao ambapo ameahidi kuzipatia ufumbuzi hivi karibuni.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali imejidhatiti kufanya maboresho makubwa ya kimiundombinu na rasilimali watu katika sekta za uchukuzi ili kuiwezesha sekta hiyo kuongeza ajira na kukuza uchumi wa nchi.

Prof. Mbarawa amesema hayo mara baada ya kukagua Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) na kusafiri wa boti kutoka Dar es Salaam kwenda Zanzibar ikiwa ni mkakati wa kupata taarifa sahihi kuhusu hali ilivyo sasa kutoka  kwa abiria na waendeshaji wa vyombo vya majini.

Amesema Serikali itaboresha Bandari ya Dar es Salaam ili kupunguza urasimu usio wa lazima na kuwawezesha abiria na boti kukaguliwa kwa haraka na kuondoka kwa muda unaotakiwa.

‘Tutahakikisha kuwa idadi ya manahodha na wahandisi wa vyombo vya majini wazalendo inaongezeka ili mkakati wa kuboresha usafiri wa majini hapa nchini uwiane na uwepo wa wataalam wa uhakika’ amesema Prof. Mbarawa.

Waziri huyo wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano amesema Serikali ina mpango wa kujenga meli mpya za kisasa katika Ziwa Victoria ili kuhamasisha wasafirishaji katika sekta ya usafiri majini kuwa na vyombo vya kisasa na hivyo kupunguza gharama za usafiri.

Katika hatua nyingine Prof. Mbarawa amekagua Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) ambapo amesisitiza kuwa Serikali itaunga mkono juhudi zinazofanywa na Chuo hicho katika kutoa mafunzo wa marubani wa ndege ili kuongeza idadi ya marubani wazalendo.

‘Mpango wetu wakukunua ndege mpya unaendana na kuwezesha Chuo hiki chenye kufundisha marubani ili tuwe na marubani wazalendo wa kutosha’ amesisitiza Prof. Mbarawa.

Amewataka wafanyakazi wa Chuo hicho kufanya kazi kwa uzalendo, ubunifu na kuzingatia matokeo ili kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanayokwenda haraka.

Naye Mkuu wa Chuo hicho Profesa Zacharia Mganilwa amemhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuwa chuo hicho kitashirikiana na Shirika la Reli Tanzania (TRL), Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA), Kampuni hodi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) katika kupata utaalam wa kisayansi katika mradi wa ujenzi wa reli ya kati ya Kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza.

Serikali imejipanga kujenga chuo cha kisasa cha Usafirishaji kwa kushirikiana na Jamhuri ya Watu wa China ikiwa ni mkakati wa kukifanya chuo hicho kuwa chuo mahiri katika upande wa Afrika Mashariki na Kati.

Zaidi ya Shilingi trilioni 4 zimetengwa na Serikali katika bajeti ya mwaka huu ili kuimarisha miundombinu ya usafiri wa Angani, barabarani, relini na majini.